MWANAFUNZI RAIA WA KIMAREKANI AHUKUMIWA KIFUNGO CHA MIAKA 15 KOREA KASKAZINI
Mahakama ya Juu nchini Korea
Kaskazini imemhukumu mwanafunzi Mmarekani kifungo cha miaka 15 jela na
kazi ngumu, vyombo vya habari vya serikali vimeripoti.
Otto Warmbier, 21, alikiri kuiba bango la kisiasa katika hoteli alimokuwa akiishi na kundi la watalii mjini Pyongyang.
Alikamatwa Januari alipokuwa akijaribu kuondoka Korea Kaskazini.
Baadaye alijitokeza kwenye runinga akionekana kukiri makosa hayo na kusema kundi moja la kanisa lilikuwa limemuomba abebe kitu cha kukumbuka kutoka kwa safari yake.
Korea Kaskazini wakati mwingine huwafunga jela wageni kama njia ya shinikizo kwa mataifa yanayoipinga.
Warmbier, 21 alikuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Virginia.
Wakati wa kukamatwa kwake tarehe 2 Januari, shirika la habari la serikali la KCNA lilisema alikuwa ameingia Korea Kaskazini akiwa na lengo la “kuvuruga umoja wa taifa” na kwamba alikuwa amedhibitiwa na kuelekezwa na serikali ya Marekani.
Akiongea kwenye runinga Februari, huku akitokewa na machozi, alisema alitenda “kosa kwa kuondoa bango la kisiasa kutoka eneo la kusubiri wafanyakazi katika hoteli ya Yanggakdo”.
“Lengo langu lilikuwa kudhuru kujitolea na bidii ya watu wa Korea. Hili lilikuwa lengo la kijinga sana,” alinukuliwa akisema.
Alisema ndilo kosa kubwa kabisa alilowahi kulifanya maishani.
Category:
0 comments