WALIMU KUPANDA DALADALA BURE TANZANIA
Mwalimu akiwa kazini |
Hatimaye walimu katika jijini Dar es Salaam nchini Tanzania wataanza kusafiri bure bila ya kutozwa nauli.
Mkuu wa wilaya ya Kinondoni Mh Paul Makonda |
Mkuu wa wilaya ya Kinondoni Paul Makonda ameutangaza uamuzi huo wa walimu kusafiri bure wanapoelekea na kurudi kazini, baada ya ombi alilolitoa kuwaombea walimu walioko katika wilaya yake, kwa wamiliki wa mabasi hayo ya usafiri maarufu kama daladala, kukubaliwa.
Uamuzi huo utaanza kutekelezwa kuanzia Machi saba, lakini muda wao wa kusafiri bure utaanzia saa kumi na moja na nusu alfajiri hadi saa mbili alfajiri na kuanzia saa tisa hadi saa kumi na moja jioni. Na kwamba zaidi ya muda huo watalipa nauli.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Madereva mkoa wa Dar es Salaam Shabani Mdemu amesema wamekubali kuwabeba walimu bure, lakini kwa shartu wasipande wengi katika basi moja.
Tayari wanajeshi wamekuwa wakisafiri bure katika daladala bila kutozwa nauli, huku wanafunzi nao wakilipia usafiri huo nusu ya nauli.
Hata hivyo, baadhi ya wamiliki wa daladala ambao hawako katika umoja huo wameitupia lawama serikali kwa kushindwa kutatua ufumbuzi wa matatizo ya walimu na baadaye kuwatupia mzigo wao.
Wamesema ufumbuzi ni kutafuta fedha wanazodaiwa na walimu na kuwalipa ili nao waweze kumudu maisha yao.
Category:
0 comments